RSS Feed

Tag Archives: watoto

Kukata tamaa: Je, ni hulka ya Watanzania?

Posted on

“Sitaenda kwenye maandamano. Hata tukiandamana hakuna kitakachobadilika.” Iliuwa kauli ya kwanza ya Mtanzania mmoja. Mwingine naye, “Nendeni tu kwenye mkutano. Mtakalolizungumza lolote kwangu ni sawa tu. Hata hivyo hiyo mikutano haina maana yoyote.” Sasa iliyonishangaza na kunikera zaidi ilikuwa hii:

“Hii ni Tanzania bwana. Mtapiga kelele weeee ila hakuna kitakachofanyika. Kujihusisha kwenye mambo ya siasa ni kazi bure. Wewe fanya mambo yako. Tafuta chakula cha familia yako. Jitafutie maendeleo yako mwenyewe. Achana na mambo ya kitaifa. Acha kabisa kuongelea siasa za nchi.”

Hizi ni kauli za watu waliokata tamaa. Ni kauli za Watanzania wengi: vijana na hata wazee. Ni watu waliochoka. Mbele yao wanaona bahari na nyuma yao majeshi ya Farao. Wamefika mwisho. Hawana tumaini. Ila kauli hizi si za kupuuza hata kidogo. Hizi ni kauli-sumu kwa taifa ambalo linataka kupiga hatua ya kimaendeleo.

Ni kauli zenye nia ya kuzima dhamira za watu ambao wangependa kudai haki zao. Ni kauli ambazo viongozi wazembe, wavivu na wabadhirifu wangependa kuzisikia. Kibaya zaidi: hizi ni kauli ambazo zaweza kuleta kizazi cha watu waoga, wasiopenda kuhoji nchi yao inaendeshwaje. Ni mawazo-mgando. Mawazo hatari!

Mtanzania yeyote anayetoa kauli za hivyo usidhani kuna siku atamkemea mtoto wake asijihusishe na wizi wa mali za umma. Na wala sidhani kama watoto wa mtu mwenye mawazo kama haya wanaweza kufikiri kwamba wizi wa mali za umma ni jambo baya. Tutaleta Tanzania kizazi kisicho na maadili kwa sababu kizazi chetu kimekuwa ni chenye kupuuzia.

Shime Watanzania, tuamke! Zi wapi nyimbo zetu za kizalendo? Zi wapi kauli zetu za ukombozi? U wapi ujasiri wetu wa kale? Ni nini kimetupata?

Usafiri wa umma (mijini) Tanzania

City public transport in Tanzania is not suitable for children, the elderly and diabled

City public transport in Tanzania is not suitable for children, the elderly and disabled

Leo wakati nakuja kazini nilitumia usafiri wa daladala. Pale nilikopandia daladala kulikuwa na akina mama ambao umri wao ulikuwa umeenda kidogo. Kwa kweli niliwahurumia. Hakuna jinsi ambavyo unaweza kupanda daladala bila kusukumana. Na kwa umri wa hao mama zangu nilikuwa na wasiwasi kwamba kwa kweli ingewawia ngumu kupata usafiri.

Ukijaribu kuangalia usafiri wetu wa umma hasa ule wa mijini utakubaliana na mimi kwamba si usafiri ambao watoto, wazee na wenye ulemavu wanaweza kuutumia bila matatizo.

Si wazee wengi wanaoweza kupanda gari kwa kupitia dirishani. Si watoto wengi wanaweza kusukumana ili kupenya kwenye mlango na kuingia ndani ya basi. Wala si walemavu wengi wanaoweza kubanana kwenye gari ili waweze kufika waendako.

Hili ni tatizo la kiuongozi kwani kuwa na usafiri wa kistarabu mijini inawezekana. Inaweza kufanyika kirahisi zaidi kuliko KILIMO KWANZA.

Follow

Get every new post delivered to your Inbox.