Kwa wale mnaofuatilia mambo ya Tanzania kwa karibu mtakumbuka kwamba hivi karibuni taifa lilikumbwa na mgao wa umeme. Japo ni vigumu kusema kama mgao huu umeisha ua la ila hali kwa sasa hivi (hasa hapa katika jiji la Dar es salaam) hali kidogo ime-stabilize.
Katika mazingira ya Kiafrika na hasa ya Kitanzania mambo mengi hufanywa kwa mtindo wa zimamoto. Miali ya moto ikishazimwa huwa hatuhangaiki hata kidogo kwenda kuchunguza chanzo cha moto ili kuzuia majanga mengine kama hayo kutokea siku za usoni. Tunakaa halafu tunakuja kukutana na tatizo kama lile lile na tunalitatua kwa style ile ile kana kwamba hatujifunzi kutokana na matatizo.
Wakati hali ya umeme nchini ikiendelea kutengemaa, ingawa ni kwa muda tu, ningependa kutoa ushauri wangu wa bure kwa wahusika. Ninafanya hivyo nikijua kabisa kwamba blog hii inasomwa na viongozi na watu wengi walio katika nafasi za maamuzi serikalini (kwa taarifa nilizo nazo). Kwa Mh. Ngeleja ningependa kutoa ushauri kwamba hiki si kipindi cha kupumzika. Wakati hali ikiwa inaonyesha dalili nzuri ni wakati wa kuchakarika na kutafuta nini hasa chanzo cha kukatikatika kwa umeme hapa nchini na ukae na wataalamu wako mtengeneze mpango-mkakati wa kutatua tatizo hili mara moja na ya mwisho.
Huko mbele tunakoelekea wataalamu wa mazingira wanasema wazi kwamba hali ya hewa hasa kwa bara la Afrika haitakuwa nzuri. Maeneo mengi yatakumbwa na ukame usio wa kawaida. Mvua hazitakuwa za kutegemewa tena. Hiyo lazima itufanye sisi tulio katika sekta ya nishati kuwaza mara mbili — lazima tuwe na vyanzo vingine vya umeme ambavyo siyo vile vinavyotegemea maji (Hydro-power). Lazima tuje na njia mbadala na endelevu za kutatua tatizo hili. Tunaweza hata tukaanza kutengeza vinu vya umeme karibu na maeneo ambako makaa ya mawe yanapatikana. Tuanze pia kuwaza kuhusu madini yetu ya Uranium tuliyo nayo kama tunaweza kuyarutubisha na kuzalisha umeme kutokana na nguvu ya kiatomia (atomic). Tutafute (kwa dhati) wataalamu katika eneo la kuzalisha umeme utokanao na gesi. Kuna maeneo ya Songosongo kule nasikia kuna kiasi fulani cha gesi ambacho kinaweza kuzalisha umeme.
Pamoja na njia hizo hapo juu lakini pia tusisahau kuwa na mitambo mizuri ya dharura ya kuzalisha umeme ambayo ina uwezo mkubwa wa kuzalisha umeme kuliko uwezo wetu tulio nao wa kuzalisha umeme kwa sasa.
Kwa sasa tuna uwezo (endapo vyanzo vyote vitafanya kazi katika kama inavyotakiwa) wa kuzalisha megawatt zipatazo 660. Tukiweza kununua mtambo mkubwa wa kufua umeme wenye uwezo wa kuzalisha megawatt, say, 800 kwa wakati mmoja na tukahakikisha huu mtambo uko katika hali nzuri na standby tutasahau kabisa tatizo la umeme.
Kwa ufupi ni kwamba tunatakiwa kujifunza kutokana na historia na tusiwe watu wa kurudia historia. Naamini hili liko ndani ya uwezo wa serikali yetu tukufu. Tanzania isiyo na tatizo la umeme inawezekana.
KILIMO KWANZA!


